Thursday, April 17, 2014

WAFANYABIASHARA WAGOMA KUFUNGUA MADUKA


 Mtaa wa Uhindini moja ya mitaa ambayo siku za kawaida huwa na msongamano wa watu mjini Iringa.

 Mtaa wa Mantigo au Miyomboni kati ya mitaa ambayo nayo siku za kawaida huwa na msongamano mkubwa wa watu mjini Iringa.
 Hapa ni katikati ya mji wa Iringa- panaitwa mtaa wa Kongo, eneo la stendi ya daladala, nako hali ndiyo kama hii unavyoiona- maeneo haya huwa na mrundikano mkubwa wa watu mjini Iringa.

hapa ni eneo la barabara Pacha za Mwembetowa Stendi kuu, nako hali halisi kama inavyoonekana maduka nayo yamefungwa.
WAFANYABIASHARA mkoani Iringa wamegoma kufungua maduka, huku biashara mbalimbali za kiuchumi zikisitishwa, kwa kile wanachodai kuwa kufanyiwa usumbufu uliokithiri na baadhi ya watumishi wa wanaitaka Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA), zikiwemo mzigo wa kodi unaowaelemea.
Mgomo huo ambao umeanza mapema alfajiri ya siku ya leo, huku baadhi ya wanaofungua huduma za kibinadamu nao wakishinikizwa kutotoa  huduma hizo, unachangiwa pia na mashine za Kielectreonic za EFD za kutolea Stakabadhi pindi tu mteja anaponunua bidhaa .
Wakizungumzia mgomo huo baadhi ya wafanyabiashara hao wamesema mgomo huo umefikiwa baada ya kutosikilizwa kilio chao, huku kukiwa na mkanganyiko kati ya wafanyabiashara wa kariakoo jijini dar es salaam kusitishiwa utaratiubu huo mpya wa TRA wakati wao wa mikoani wanaonunua bidhaa zao zote kariakoo wakitakiwa kuwa na kumbukumbu za manunuzi.
"Hebu ona ndugu mwandishi, kule Kariakoo wanunuzi wanaotuuzia mali hizi zote kutokja mikoa wamepewa muda wa kuendelea na utaratibu wao wa zamani wa kutotumia mashine za EFD, lakini sasa sisi tunapokuja huku mikoani hawa TRA wanasema hawaelewi hilo tunatakiwa kuambatanisha kwenye malipo manunuzi yetu, sasa sisi tunatoa wapi wakati wafanyabiashara wakubwa dar hawatupi risiti??," Alihoji Tito Kalole.
James Mdegipala mmoja wa wafanyabiashara hao amesema ipo haja kwa TRA pia kuwasikiliza malalamiko yao juu ya gharama kubwa za ununuzi wa mashine hizo.
Makey Masharo amesema wataendesha mgomo huo mpaka malalamiko yao yatakaposikilizwa kwani baadhi ya wafanyabiashaea wameingiwa na hofu juu ya tishio la upandishaji wa kodi kwa  asilimia 18.
Jackson Kalole naye amesema serikali inapaswa kushirikiana na wadau wake pindi inapotaka kufanya mabadiliko, hasa yanayohusu uchumi wa nchi ili kuondokana na changamoto hizo, kwani licha ya kuwepo kwa kodi zaidi ya 9 kwa mfanyabiashara mdogo wa duka, kumekuwa na tatizo la elimu juu ya ongezeko la kodi hizo.

Aidha wafanyabiashara hao wamesema hawapo tayari kufungua maduka yao, hadi pale serikali itakapoona umuhimu wa kukaa meza moja na wao ili kumaliza changamoto hizo.

Naye Lukas Mwakabungu mwenyekiti wa chama cha wafanyabiashara, wenye viwanda na wakulima TCCIA amesema chemba hiyo haihusiki na mgomo huo na kuwa atakaa na wafanyabiashara hao ili kutambua sababu za wao kugoma.
Mkuu wa mkoa wa Iringa Dr. Christine Ishengoma amewataka wafanyabiashara hao kufungua maduka yao, kwa madai kuwa huo ni mkumbo wa baadhi ya vijana wanaochochea wenzao kutofungua maduka.
Hata hivyo wafanyabiashara hao wametawanywa na jeshi la polisi mara tu walipojaribu kutaka kukusanyana ili kujadili hatma ya tatizo hilo, ambapo wameitaka serikali kuona hasara inayoingia kwa kushindwa kukusanya kodi katika siku watakazokuwa wamesusia kufungua maduka na kutoa huduma kwa jamii.

MWISHO.

Jumamosi, 4 Januari 2014

"FAWE na TUSEME" MARUFUKU WATOTO KUTUMIKISHWA KATIKA AJIRA


 Baadhi ya watoto washiriki wa kongamano la kambi lililoandaliwa na shirika la FAWE kwa kushirikiana na UNICEF chini ya mradi wa TUSEME, kambi iliyowekwa katika shule ya sekondari JJ. Mungai katika Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa.
Bi. Neema Kitundu- mratibu wa FAWE Taifa akisikiliza maoni ya watoto katika kambi iliyowakutanisha watoto wa shule za msingi kutoka Wilaya sita, - Wilaya ya Makete, Mbeya Vijijini, Mtwara, Temeke, Mufindi pamoja na Iringa vijijini.
 Bi. Sophia Komba mmoja wa viongozi wa mradi wa FAWE akizungumza na jopo la watoto wa shule za msingi kutoka katika Wilaya sita nchini, katika kambi iliyofanyika katika shule ya sekondari JJ. Mungai Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa.
 Baadhi ya watoto washiriki wa kongamano la kambi lililoandaliwa na shirika la FAWE kwa kushirikiana na UNICEF chini ya mradi wa TUSEME, wakionyesha ubunifu wao wa kuchora michoro inayoendana na mafunzo ya kupinga ukatili na unyanyasaji wa watoto, ambao unachangia baadhi yao kuikosa elimu.
 Baadhi ya watoto washiriki wa kongamano la kambi lililoandaliwa na shirika la FAWE kwa kushirikiana na UNICEF chini ya mradi wa TUSEME, kambi iliyowekwa katika shule ya sekondari JJ. Mungai katika Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa.
 Baadhi ya watoto washiriki wa kongamano la kambi lililoandaliwa na shirika la FAWE kwa kushirikiana na UNICEF chini ya mradi wa TUSEME, kambi iliyowekwa katika shule ya sekondari JJ. Mungai katika Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa.
 Baadhi ya walimu ambao waliambatana na wanafunzi wao katika kambi hiyo wakisikiliza maoni ya wanafunzi hao juu ya ukatili wanaofanyiwa.
 Watoto kutoka Wilaya ya Temeke wakitoa ushuhuda kupitia maigizo kama ni sehemu ya ushiriki wao katika kambi hiyo.

 Watoto washiriki wa kambi la wanafunzi kutoka Wilaya sita nchini wakitoa ushuhuda juu ya vitendo vya ukatili vilivyopo katika jamii wanamoishi.

SHIRIKA la FAWE chini ya mradi wake wa TUSEME nchini Tanzania  limepiga marufuku mtindo wa baadhi ya wazazi na walezi kuwatumikisha watoto wenye umri wa kwenda shule, katika shughuli mbalimbali ambazo ni kikwazo katika elimu.
Hayo yamezungumzwa na mratibu wa FAWE nchini Bi. Neema Kitundu katika kongamano la watoto   wa shule za msingi kutoka Wilaya tisa nchini, ambapo amesema tatizo la watoto kutumikishwa bado lipo katika Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa, pamoja na Wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya.
Bi. Kitundu amesema tatizo hilo halina tofauti na ukatili wa kijinsia, na kuwa hali hiyo imeshamiri sana katika Wilayani Mufindi ambapo watoto hutumikishwa kama vibarua katika mashamba ya Chai, huku wengine wakitumiwa katika ajira za kazi za nyumbani.
Aidha Bi. Kitundu amesema katika Wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya nao wanaukatili kwa watoto hao wadogo, na kuwa wao huwatumia watoto katika mashamba ya Mpunga, jambo linalowafanya wakose kwenda shule.
“Tumeona bado kuna changamoto  kubwa kwa watoto hawa, na katika wilaya tunazozifanyia kazi tumetambua Wilaya ya Mufindi inawatumikisha watoto katika mashamba ya Chai, huku Wilaya ya Mbarali watoto wengi wanafanyishwa kazi katika mashamba ya Mpunga, jambo hili ndugu zangu linakwamisha sana sekta ya elimu, na halina tofauti na ukatili wa kijinsia, kwani watoto hawa wanaikosa fulsa muhimu ya elimu,” Alisema Kitundu.
Amesema baadhi ya watoto wamekuwa wakitoroka shule na hata kutokwenda kabisa na kukimbilia katika ajira hizo na hivyo kupoteza muda wa masomo, jambo ambalo linaashiria kukosekana kwa elimu kwa watoto hao na hivyo Taifa kuwa na watu wasio na elimu.
“Katika Wilaya ambazo tumezifikia tatizo la ajira za utotoni tumetambua bado zipo kwa Wilaya ya Mufindi na Mbarali, na wengi wetu hasa tunaotoka Dar es Salaam tumekuwa na dhana ya kuwa wasichana wa kazi za ndani wazuri wanatoka Mufindi Iringa, na kule Mbarali wao wanajihusisha sana na kilimo cha Mpunga, na wakati wa kilimo watoto wengi wanashinda mashambani, na hata wazazi wapo radhi kuomba ruhusa shuleni kwa kisingizio kuwa mtoto swake anaumwa kumbe anamfanyisha kazi za shambani, si wavulana si wasichana” Alisema
Amesema FAWE kwa kushirikiana na UNICEF walifanya kazi kwa wilaya kumi, na sasa wameanza na Wilaya sita ambazo ni Wilaya ya Makete, Mufindi, Njombe, Mbeya vijijini, Iringa Vijijini na Wilaya ya Mbarali.
Amesema mradi FAWE kwa kushirikiana na UNICEF umeweza kuleta mafanikio makubwa, kwa kupunguza tatizo la wanafunzi wa kike kuacha masomo kwa kupata mimba, ambapo  mwaka 20006 kabla mradi haujaanza kufanyakazi mimba zilikuwa zaidi ya 400 kila mwaka kwa shule za msingi pekee, na shule zilizokuwa ndani ya mradi wa FAWE mimba zilikuwa 166 kwa mwaka, na mafanikio yamepunguza tatizo hilo la mimba hadi ambapo mwaka 2013 mimba zimebaki tatu pekee.
Naye mwasisi wa FAWE nchini Profesa Penina Mrama amesema FAWE kwa kushirikiana na TUSEME inamsaidia mtoto kupata elimu ya utambuzi wa haki zake za msingi na kuondoa ubaguzi baina ya watoto wa kike nawa kiume.
Profesa Penina amesema kupitia mradi wa FAWE na TUSEME  wameweza kuwaokoa watoto wengi ambao walikuwa tayari wameikosa elimu, na sasa wamejikita zaidi kulielimusha kundi hilo kutambua haki zao ili waweze kuzitetea.
Na kuwa shirika limekuwa likitoa afua za kusaidia sekta ya elimu kwa kujenga miundombinu wezeshi kama Maktaba, Maabara, Mabweni y Chakula, utoaji wa Vitabu nk. yote hayo yakiwa yamelenga kuyafanya mazingira ya elimu kuwa rafiki kwa wanafunzi ili kuvutia na kuipata elimu pasipo na vikwazo vovyote. 
Aidha Profesa Penina amesema pia mradi unapingana na vitendo vya ukatili vinavyochangia mtoto kushindwa kupata elimu, zikiwemo ajira pingamizi kwa sekta ya elimu.
Hata hivyo shirika la kazi duniani (ILO) katika ripoti yake iliyotolewa mjini Geneva kuna zaidi ya watoto milioni 10.5 duniani wanatumikishwa kazi za nyumbani katika  mazingira magumu.

Katika ripoti hiyo Shirika la Kazi Duniani ,limeeleza kwamba watoto hao wanafanya kazi za usafi, wanapika,wanatunza bustani na pia wanafanya kazi ya uyaya, hiyo ikiwa haina tofauti kabisa na ripoti ya FAWE katika Wilaya zake inazozifanyia kazi, ambako changamtoto hizo za kazi kwa watoto nazo zimejitokeza kwa kiwango kikubwa.

ILO ilienda mbali zaidi na kusema katika ripoti yake kuwa watoto milioni sita na nusu  wanaofanyishwa kazi za majumbani wana umri kati ya miaka 5 na 14  na zaidi ya asilimia 71 ni wasichana.
Pia ILO ilibainisha kuwa watoto wengi wanaoajiriwa majumbani mara nyingi hawalipwi ujira stahiki na waajiriwa wao, huku baadhi ya waajiri wakidiliki hata kuwabagua , jambo linalojenga dhana potofu katika vichwa vya Taifa hilo la kesho.

Na hali hiyo ya ajira kwa kundi la watoto isipopigiwa kelele inaweza kuongezeka zaidi kila mwaka kutokana na mahitaji  ya watumishi wa nyumbani, kutokana na ukweli kuwa asilimia kubwa ya wananchi wanajishughulisha na kazi mbalimbali na hivyo kuwa na uhitaji mkubwa wa wafanyakazi wa kazi za nyumbani.
Huenda hali hiyo ya ajira kwa kundi la watoto wadogo likaongezeka zaidi na zaidi kutokana na wanawake wengi kupata kazi nje ya nyumba  hali inayotofautiana na siku za awali ambapo mwanamke alionekana kuwa ndiye muhusika mkuu wa kazi za nyumbani za kuihudumia familia.

MWISHO

Jumatatu, 30 Desemba 2013

BARABARA YA HIFADHI YA RUAHA YAKWAMISHA UTALII


 Wadau wa sekta ya Utalii wakisikiliza jambo katika moja ya vikao vya kujadili mikakati ya namna ya kuendeleza sekta hiyo ambayo ni kiini cha Pato la Taifa.
 Mmmoja wa viongozi wa mradi wa SHICs unaojihusisha na kuendeleza utalii wa mila na tamaduni mikoa ya Kusini (Iringa) akifafanua jambokatika ukumbi wa chuo kikuu cha Iringa, ambapo wadau wa sekta hiyo ya Utalii walikutana.
Yan Kuva meneja wa mradi wa SHICs unaojihusisha na kuendeleza utalii wa mila na tamaduni mikoa ya Kusini (Iringa) akifafanua jambo katika chuo kikuu cha Iringa, ambapo chuo hicho kimepewa dhamana hiyo.
 
MIUNDOMBINU mibovu, ajira za kindugu zisizozingatia utaalamu na kauli zisizofaa, ni moja ya vikwazo vinavyoikwamisha sekta ya utalii mkoani Iringa, licha ya mkoa huo kupewa heshima ya kuwa kitovu cha Utalii nyanda za juu kusini.
Hayo yamezungumzwa na wadau wa sekta ya Utalii mkoani Iringa, katika kikao chenye lengo la kuendeleza Utalii wa mila na tamaduni za jadi, lengo likiwa ni  kuwavutia watalii walio wengi kufika mkoani humo kujifunza maisha ya awali ya makabila ya mkoa wa Iringa, na hatimaye fedha za mapato ya watalii kusaidia kukuza uchumi na pato la Taifa.
Steven Mhapa ambaye ni mwenyekiti wa halmashauri ya Wilaya ya Iringa na mdau wa utalii amesema ubovu wa barabara inayoelekea katika Hifadhi ya Taifa ya Ruaha ni changamoto kubwa katika kuyafikia malengo ya kuinua sekta ya utalii mkoni Iringa.
“Tunafahamu barabara barabara ni kiungo muhimu sana katika kuwafikisha watalii katika hifadhi, sasa barabara yetu ya Ruaha si rafiki kabisa kwa vivutio vya utalii, na kutokana na hali hiyo baadhi ya watalii wenye uwezo huamua kukodi usafiri swa anga yaani Ndege, huku wenye kipato cha kawaida wakitumia usafiri wa barabara, ambapo hao wamekuwa wakilalamikia sana barabara hiyo na hivyo pindi wanapomaliza utalii wao huwa hawarudi tena, ipo haja ndugu zangu kujipanga vyema hasa katika miundombinu ya barabara,” Alisema.
Afisa utamaduni Wilaya ya Iringa Bi. Joyce Nachilima amesema hata masuala ya utandawazi nayo yanabainishwa kuwa yanachangia baadhi ya vijana kutohitaji tena mambo ya mila na tamaduni za jadi, kuanzia mavazi na hata vyakula, wakihitajika vile tu vinavyokwenda na wakati.
“Vijana wetu wengi siku hizi wanafikilia tu kutunga nyimbo za Bongo fleva ambazo ndiyo zinaitwa za kizazi kipya, na unapowaambia wabuni nyimbo za jadi kama Mangala na Kiduo nyimbo za asili kwa makabila yao wao wanaona kama ni masauala yaliyopitwa na wakati, sasa jambo hilo linakuwa ni gumu sana kufanikiwa maramoja katika sekta ya Utalii wa tamaduni,” Alisema.
Naye Hawa Mwechaga afisa utalii Wilaya ya Iringa amesema wananchi mkoani Iringa wanapaswa kuanza wenyewe kuvitangaza vivutio vya mila na tamaduni za makabila yao, ikiwa pamoja na kuendelea kuvaa mavazi aina ya “Migolole” ambayo yalivaliwa na machifu wa kabila la Wahehe, na kuacha tabia ya kuiga mavazi ya makabila mengine kama ya Wamasai.
Hata hivyo Jimson Sanga ambaye ni katibu wa mradi wa kuendeleza Utalii wa mila na tamaduni mkoa wa Iringa, amesema wananchi mkoani humo wana fulsa nyingi katika kuboresha utalii, hasa kubwa ikiwa ni kipaumbele cha mkoa wa Iringa kupewa heshima ya kuwa ni kitovu cha Utalii nyanda za juu kusini.
MWISHO

Jumatano, 18 Desemba 2013

KATIBU TARAFA AHIMIZA UJENZI WA VYOO BORA


 KATIBU tarafa wa tarafa ya Pawaga Bw. Nasson Mwaulesi (Mwenye suti nyeusi aliyesimama) akisisitiza jambo katika mkutano huo ambao pia ulihudhuriwa na Waziri Willium Lukuvi.

 Waziri Lukuvi akijaribu moja ya Pikipiki huku katibu tarafa Mwaulesi akiangalia kitendea kazi hicho, ambapo Waziri huyo alikabidhi Pikipiki nne ambazo kati yake zilipelekwa  tarafa ya Isimani na Idodi.
 
KATIBU tarafa wa tarafa ya Pawaga Mkoani Iringa Bw. Nasson Mwaulesi amewataka wananchi kujenga vyoo bora na vya mfano ili kuepukana na magonjwa ya mlipuko kama Kipindupindu.
Akizungumza na wananchi wa kijiji cha Kimande, katibu tarafa huyo amesema hakuna njia mbadala ya kukwepa magonjwa ya matumbo pasipo kuboresha mazingira ukiwemo ujenzi wa vyoo hivyo bora.
Aidha Mwaulesi amesema ili kufanikisha mpango huo na kuondokana na vyoo duni atahakikisha ofisi ya afya wilaya ya Iringa inapeleka mchoro wa choo bora kinachotumia ujenzi wa gharama nafuu, ukiwa ni msisitizo wa kuachana na matumizi hayo ya vyoo duni .
"Kuna vyoo vya ajabu sana hapa, vilivyo vingi hata mlango havina, wengine wameweka magunia katika vyoo vyao, na baadhi ya nyumba hazina vyoo kabisa, uongo??...Sasa jamani achaneni na tabia hiyo, kwani uzuri wa nyumba ni choo," Alisema.
Pia aliwataka wananchi na ofisi za vijiji vyote 12 vya tarafa hiyo ya Pawaga kukamilisha ujenzi wa vyoo hivyo ifikapo April mwaka 2014, ambapo alimuagiza mkuu wa Polisi tarafa ya Pawaga kuwachukulia hatua za kisheria wananchi wote watakaokaidi agizo hilo.
Hata hivyo mbunge  wa  jimbo la Isimani ambae ni  waziri  wa nchi  ofisi  ya  waziri mkuu  sera na uratibu wa bunge Mh. Wiliam Lukuvi akikabidhi  gari  la  wagonjwa  lenye  thamani  ya  zaidi  ya Tsh milioni 180 katika kituo cha afya  Kimande Pawaga  amewataka wananchi hao kujiunga na mpango wa huduma ya afya jamii (CHF) ili kuepukana na gharama kubwa za matibabu.
Waziri Lukuvi pia alikabidhi Pikipiki nne zenye thamani ya zaidi ya shilingi Milioni saba, ambapo Pikipiki mbili zilikuwa ni ahadi ya mh. rais Jakaya Kikwete na mbili zilinunuliwa na Waziri Lukuvi, kwa ajili ya ufuatiliaji wa miundombinu ya mradi wa maji bomba.
Katika kuhakikisha wananchi hao hawana vyoo bora Waziri Lukuvi alishindwa kumpata mwananchi hata mmoja mwenye choo bora cha mfano katika kijiji hicho, hatua iliyoonyesha baadhi ya wananchi hao kutolitilia mkazo suala hilo la ujenzi wa vyoo bora.
MWISHO

No comments:

Post a Comment