Thursday, December 26, 2013

WATAKA "ATM MASHINE" ZA KONDOMU ZA KIKE


Moja ya mashine za kutolea mipira ya kiume Kondom- ATM Mashine ambazo zimewekwa katika maeneo mbalimbali ya starehe ili kurahisisha upatikanaji wa zana hizo, lengo likiwa ni kuzuia maambukizi mapya ya Virus Vya Ukimwi- VVU.
 Jengo la halmashauri ya Wilaya ya Kilolo-m Mkoani Iringa

KUKOSEKANA kwa mashine za kutolea mipira ya kondomu za kike, ikiwa pamoja na kondomu hizo kutopatikana kwa urahisi, kumeifanya jamii ione serikali inawajali zaidi wanaume kwa kuwalinda kuliko kundi la wanawake ambao wamekuwa waathirika wakubwa wa ugonjwa huo.

Farida Shirima mmoja wa wananachi mkoani Iringa amesema wanaume wamepewa kipeumbele katika kulindwa, kwa kutengenezewa mashine maalumu zinazotoa huduma ya kondomu hizo “ATM Kondom Mashine” huku kila eneo  zana hizo zikipatikana kwa urahisi, hali ambayo ni tofauti kabisa na upande wa kondom za kike ambazo hata katika baadhi ya vituo vya huduma za afya hakuna.

Nao madiwani wa halmashauri ya Wilaya ya kilolo, wakati wakijadili masuala mbalimbali ya maendeleo na uchumi, vikiwemo vikwazo vya maendeleo kama ugonjwa wa ukimwi, wamesema ipo haja kwa serikali kuagiza kondomu za kike ili nazo zipatikane kwa wingi na hivyo wanawake kuwa na fulsa katika kujikinga na magonjwa ya zinaa na ukimwi.

Wakizungumzia hali hiyo madiwani hao wamesema upatikanji wa mipira hiyo ya kike ni shida tofauti na kondomu za kiume ambazo licha ya kupatikana kila mahali pia imetengenezewa mashine maalumu kwa ajili ya kutoa huduma hiyo “ATM Kondom Mashine” ambazo zimewekwa katika maeneo mbalimbali ya Starehe.

Akilalamikia hatua ya kukosekana kwa Kondomu za kike katika maeneo yaliyo mengi, mmoja wa madiwani Anna Kulanga amesema serikali imewekeza nguvu zake nyingi katika kondomu za kiume kwa kuhakikisha zinapatikana kwa urahisi, huku kondomu za kike zikisahaulika na kuwa nadra sana upatikanaji wake.

Kulanga amesema tatizo hilo linachangia wanawake kushindwa kujikinga na maambukizi mapya ya VVU, kutokana na kukosa zana hizo, ambazo zimesahaulika baada ya serikali kuelekeza nguvu zake kwa kutenga bajeti katika mipira hiyo ya kiume.

“Mh. Mwenyekiti sisi wanawake katika kitengo hiki cha ukimwi inaonekana kama tumesahaulika, maana hata unapokwenda katika vituo vya afya ya uzazi unapatiwa kondomu za kiume, wakati matumizi ya mipira hiyo ni hiyari ya mwanaume, atumie au laa, tunaitaka serikali ione kuna haja kubwa ya kutenga bajeti ili kuzifanya kondomu za kike zipatikane sawa kama zilivyo vya kiume,” Alisema Kulanga.

Aidha amesema wanawake waliowengi wanajikuta wakilazimika kufanya mapenzi bila kinga, na hivyo kuangamia kwa kupata maambukizi ya Virusi vya Ugonjwa wa  ukimwi, kwa madai kuwa baadhi ya maeneo ya vijijini bado kuna tabia ya mfumodume wa wanaume kuwa na wanawake wengi.

Naye mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo Joseph Muhumba amesema tatizo hilo ni kubwa kwani hata ofisi zilizo nyingi katika vyoo kumewekwa huduma hiyo ya kondomu za kiume pekee na kuitaka Halmashari kutenga bajeti ya fedha za kununulia zana hizo za kuwalinda wanawake na ukimwi.

“Kweli hili ni tatizo kubwa, ipo haja kwa serikali kuona umuhimu wa kutenga bajeti ili kuliokoa kundi hili la wanawake, nao wawe na maamuzi ya kutumia zana zao au laa, kama ilivyo kwa wanaume, tunasema wanawake ni jeshi kubwa na ukiwaelimisha wao umeielimisha jamii, basi ipo haja kuwalinda kwa kuona hawaangamii kwa ukimwi,” Alisema Muhumba.

Mratibu wa shughuli za Ukimwi Wilaya ya Kilolo Faraja Chaula alikiri kuwepo kwa uhaba wa mipira hiyo ya kike, na kuwa hata elimu juu ya matumizi yake bado haijawafikia wanawake walio wengi.

Chaula amesema katika kukabiliana na hali hiyo Halmashauri tayari imetenga bajeti ya kununua kondomu za kike katoni 109, ikiwa pamoja na kutoa elimu sahihi ya matumizi ya zana hizo,ili kuwakinga wanawake na VVU.

“Ni kweli katika shughuli za mapambano ya ukimwi wanawake ndiyo wahanga, hasa kutokana na shughuli wanazofanya ukizingatia ndiyo wenye majukumu makubwa ya kulea familia, lakini hawana maamuzi katika suala la mapenzi na changamoto kubwa kwao ni uhaba wa Kondomu za kike, lakini kwa kuanzia Halmashauri tumetenga bajeti ya kununua kondomu hizo za kike pamoja na kutoa elimu ya matumizi ya kondomu hizo,” Alisema.
MWISHO


No comments:

Post a Comment