Monday, December 31, 2012

POLISI WAWILI,MWANASHERIA WA SERIKALI; KORTINI KWA KUHARIBU UCHUNGUZI NYARA ZA SERIKALI



 ASKARI wawili wa Jeshi la Polisi pamoja na Katibu wa Ofisi ya Mwanasheria wa Serikali mkoani Iringa,wamepandishwa kizimbani baada ya kukamatwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) wakikabiliwa na tuhuma za kuomba rushwa ya sh. milioni Sita ili wawasaidie watuhumiwa wa  pembe za ndovu.

Watuhumiwa hao wamefikishwa leo mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoa wa Iringa, Consolatha Singano kujibu tuhuma  hizo za  kuomba rushwa ya sh. mil. sita kutoka kwa washitakiwa watatu wa nyara za serikali, Patrick, Raymond na Hamisi  ambao wanakabiliwa na kesi ya kukutwa na pembe za ndovu kinyume cha sheria.

Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) , Imani Nitume, akisoma jalada la kesi hiyo  namba 306 ya mwaka 2012 lenye mashitaka saba,  amesema kuwa watuhumiwa hao walitenda kosa hilo kinyume na kifungu cha sheria namba 15 (1) (a).

Alidai mahakamani hapo kuwa askari polisi mwenye namba G. 402 D/C Denis Beatus (32)  na  Joshua Bratus Mkwama (37), na Katibu wa Sheria, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Iringa, wanakabiliwa na shitaka la kwanza la kuomba rushwa ya shilingi milioni sita.

Nitume alisema Denis Beatus anakabiliwa na shitaka la pili la kupokea rushwa mnamo Desemba 12 mwaka huu kutoka kwa Diska Kshinde Gadama ili kuwasaidia ndugu zake wapate dhamana katika kesi ya kukutwa na nyaraka za serikali kinyume cha sheria.

 Aidha Nitume amesema pia Katibu wa Sheria Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, anakabiliwa na shitaka la tatu la kupokea rushwa ya silingi milioni tatu kutoka kwa Joshua Mkwama katika ofisi ya mwanasheria  Desemba 16 mwaka huu.

Mtuhumiwa mwingine, mwenye namba F 3277 D/C Karume Farijala Kunga (32) ambaye ni askari katika ofisi ya Mkuu wa Upelelezi mkoa wa Iringa (RCO), anakabiliwa na shitaka la nne la kupokea rushwa ya laki tano kutoka kwa Denis Beatus.

Diska Kashinde Gandama mkazi wa Kigamboni Jijini Dar es salaam  ambaye ni ndugu wa washitakiwa watatu wanaokabiliwa na kesi ya kukutwa na nyaraka za serikali kinyume cha sheria yeye anakabiliwa na shitaka la tano la kutoa rushwa katika kituo kikuu cha mabasi mkoa wa Iringa na kumpa Denis Beatus, kinyume cha sheria kifungu cha 15 (1) (b).

 Shitaka la sita linamkabili Denis Beatus na Kashinde Gandama  ambao wanadaiwa kutoa rushwa ya sh. 3,000,000 na kumpa Joshua Mkama ambaye ni Katibu wa Sheria Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ili kuwasaidia Patrick na wenzake katika kesi inayowakabili.

Katika shitaka la saba, Mwanasheria huyo wa Takukuru amedai kuwa, katika ofisi ya RCO,  Denis Beatus alimkabidhi Karume Farijala  rushwa ya shilingi laki tano ili kuhujumu kesi dhidi ya nyaraka za serikali inayowakabili watu watatu.

Watuhumiwa wote wamekana mashitaka yanayowakabili na mahakama imeahirisha shauri hilo hadi Januari 15 mwaka 2013, huku  wakili Alfred Kingwe anayewatetea watuhumiwa hao, akiiomba mahakama hiyo kutoa dhamana kwa wateja wake kwa kuwa  mashitaka yanayowakabili yanadhaminika.

Hata hivyo  Hakimu Singano alikubali ombi la wakili Kingwe na kutoa masharti ya dhamana ambapo kila mshitakiwa alipaswa kuwa na wadhamini wawili wenye uwezo wa kusaini dhamana ya sh. Mil. 2 na mmoja kati yao awe mwajiriwa wa serikali, huku mahakama hiyo ikizuia hati za kusafiria za washitakiwa hao.

MWISHO


No comments:

Post a Comment